| Wachezaji wa klabu ya soka ya nchini Uingereza, Chelsea wakipongezana katika moja ya michezo yao ya ligi kuu. |
Mashabiki wa soka nchini Afrika Kusini watapata fursa ya kutizama mechi za ligi kuu ya England bure, katika bustani mpya itakayofunguliwa mjini Johannesburg mwisho wa mwezi huu.
Hafla hiyo ambayo haitatoza ada yoyote, inaandaliwa kwa mara ya kwanza na mashabiki elfu kumi na mbili (12,000) wataruhusiwa kuingia ndani ya bustani hiyo ya ZOO LAKE SPORTS Club kila siku.
Mashabiki hao pia watapata fursa ya kukutana na wachezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Afrika Kusini, Bafana Bafana akiwemo Mark Fish na Lucas Radebe. Vile vile wachezaji wa zamani wa Liverpool, Robbie Fowler na mchezaji wa zamani wa Chelsea na nahodha wa Ufaransa Marcel Desailly watakuwepo.
Wakati wa hafla hiyo mashabiki watakuwa na fursa ya kuona na kupiga picha kombe la ligi kuu ya Premier ya England.